HEADER AD

HEADER AD

MSANII ATUPWA JELA MIAKA SITA KWA KUMTUKANA RAIS SAMIA

Na Daniel Limbe, Chato

MSANII wa Nyimbo za asili ya Kisukuma, Dawa Juma mkazi wa Kijiji cha Makurugusi wilayani Chato mkoani Geita, amehukumiwa kifungo cha miaka sita jela au kulipa faini ya Tsh.Milioni 10 baada ya kupatikana na hatia ya kumtukana rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan.

Hukumu hiyo imetolewa na Hakimu wa mahakama ya wilaya Chato,Amalia Mushi, baada ya mshitakiwa kukiri kosa mbele ya mahakama hiyo.

Awali mwendesha mashitaka wakili mwandamizi wa serikali,Robert Magige, ameiambia mahakama hiyo kuwa mshitakiwa alitunga wimbo wenye lengo la kumtukana matusi rais Samia Suluhu Hassan,licha ya kujua wazi kuwa kufanya hivyo ni kosa kisheria.

Amesema akiwa na nia ovu alirekodi wimbo huo na kuusambaza kwenye mitandao ya kijamii ili kupeleka ujumbe wake kwa umma huku akijinadi kuwa haogopi kukamatwa.

Mwendesha mashitaka huyo,amesema kitendo cha kuchapisha taarifa za uongo na matusi kisha kuyasambaza kwenye mitandao ya kijamii (You tube) ni kinyume na kifungu cha 16 cha sheria ya makosa ya mtandao,sheria namba 14 ya mwaka 2015.

Hata hivyo mshitakiwa baada ya kusomewa mashitaka yanayo mkabili amekiri kutenda kosa hilo, licha ya kudai kuwa hakuwa na nia mbaya kwa kuwa alikusudia kuonyesha hali ilivyo mbaya kwa jamii baada ya bidhaa kupanda bei.

Aidha baada ya mshitakiwa kukiri kosa, wakiri wa serikali Magige ameiomba mahakama hiyo kutoa adhabu kali ili iwe fundisho kwa wengine wenye lengo la kumtukana rais kutokana na sababu zao binafsi.

Akitoa hukumu, Hakimu wa mahakama hiyo,amedai kuwa kwa kuzingatia kuwa mshitakiwa hakuisumbua mahakama hiyo,kwa kukiri kosa kwa kinywa chake mwenyewe mahakama inamhukumu kifungo cha miaka sita jela au kulipa faini ya shilingi milioni 10.

Hata hivyo mshitakiwa amepelekwa gerezani kuanza kutumikia kifungo chake baada ya kushindwa kulipa faini iliyoelekezwa na mahakama hiyo.

                        

No comments