HEADER AD

HEADER AD

TARURA ILEMELA ILIVYOWAKOSHA WANANCHI BAADA YA KUKARABATI BARABARA YA IGOMBE- KAHAMA


>>Ni ile iliyokuwa mbovu kuwalazimu wananchi kusafirisha majeneza yenye miili mabegani

>>Sasa Gari, Pikipiki,Bajaji,Toroli, Mkokoteni yapita barabarani bila shida

>>Wananchi waipongeza Serikali kusikiliza kilio chao

>> Hivi karibuni, DIMA ONLINE iliripoti ubovu wa barabara ya Igombe –Kahama unavyowatesa wananchi ikiwemo kulazimika kusafirisha majeneza yenye miili mabegani


Na Dinna Maningo, Mwanza

MAISHA ya Binadamu yanahitaji furaha, pale inapotokea changamoto kadha wa kadha huondoa matumaini ya furaha,amani na kubaki katika huzuni kutokana na kero zinazomsibu au kumsumbua anapokwama kutimiza kile alichodhamilia, na wakati mwingine lawama zote huitupia Serikali akiamini imeshindwa kutatua changamoto.

Wananchi wanapotoa kero mbalimbali katika mazingira wanayoyaishi matamanio yao ni kuona Serikali inawajibika kuzitatua. Serikali inapochukua hatua basi mwananchi huyo hupata furaha na kuwa rafiki wa Serikali ama taasisi ya serikali pale inapowajibika kutatua shida zinazowakabili zinazowapa mateso baada ya kuziwasilisha katika mamlaka husika.

Wananchi wanaotumia Barabara ya Igombe – Kahama iliyopo ndani ya wilaya ya Ilemela mkoa wa Mwanza wamejawa na furaha baada ya changamoto iliyokuwa kero na mateso ya ubovu wa barabara yenye makorongo kukarabatiwa na Wakala wa Barabara za Vijijini na Mjini (TARURA) wilaya ya Ilemela mkoa wa Mwanza.

         Barabara iliyokarabatiwa hivi karibuni, baadhi ya pembezoni mwa barabara kuna mitaro iliyowekwa kipindi cha nyuma kabla ya ukarabati wa sasa wa barabara hiyo ya Igombe -Kahama

Mwenyekiti wa Mtaa wa Bujingwa, Kata ya Bugogwa Shija Habari, anaipongeza TARURA kutatua kero ya barabara hiyo na kusema kuwa TARURA ni wasikivu kwani baada ya kutoa kilio chao kupitia chombo cha habari cha mtandoni cha DIMA Online imeweza kutatua kero ya barabara iliyokuwa ikiwatesa.

Anasema baada ya barabara kukarabatiwa wananchi wakiwemo wakulima na wavuvi wanapita bila karaha wakati wanaposafirisha bidhaa zao kwa kutumia usafiri wa Pikipiki, Gari, Bajaji, Baiskeri, Toroli na mkokoteni.

‘’Tunaishukuru sana TARURA kusikiliza kilio chetu wametutengenezea barabara ambayo ilikuwa inawapa kero wananchi wanaotembea kwa miguuu na watumiaji wa vyombo vya moto, baiskeri, na mkokoteni.

‘’Sasa hivi msiba ukitokea mwili wa marehemu unasafirishwa kwa gari au bajaji tofauti na awali wakati haijakarabatiwa wananchi walilazimika kubeba jeneza lenye mwili mabegani kutoka Kituo  cha Afya Karume mwendo wa km 3 kufika Bujingwa.

Mwenyekiti huyo anaongeza kusema ‘’ Kwa sasa gari , pikipiki zinapita bila shida katika barabara ya Igombe- Kahama Kwenda Busweru iliko makao makuu ya wilaya ya Ilemela pamoja na Halmashauri ya manispaa ya Ilemea na maeneo mengineyo ‘’ anasema Shija.

         Barabara ya Igombe- Kahama iliyokarabatiwa hivi karibuni, baadhi ya sehemu za barabara haijawekewa mitaro.

Aiomba TARURA kuweka Mitaro na Karavati

Mwenyekiti huyo anasema pamoja na kuipongeza TARURA kwa kusikiliza kilio chao cha ubovu wa barabara na hivyo kuweza kuikarabati bado mitaro na karavati haijawekwa kwenye maeneo korofi ya barabara .

        Mwenyekiti wa mtaa wa Bujingwa Shija Habari, akionesha eneo la barabara ya Igombe- Kahama kabla ya ukarabati, sehemu hiyo hadi sasa imekarabatiwa ila haijawekewa kalavati. Wakati wa mvua maji hujaa na kufunika barabara na kusababisha adha kwa wapitaji na wanafunzi kushindwa kuvuka kwenda shuleni.

'' Changamoto katika barabara hiyo ilikuwa ni ubovu, ukosefu wa mitaro, karavati baadhi ya maeneo korofi. Tunaomba TARURA ijenge mitaro na karavati ili barabara iwe imara, wasipoweka msimu wa mvua barabara hiyo itaharibika na kurudi katika hali yake ya awali na kutusumbua.

'' Kuna baadhi ya maeneo katika barabara hiyo panahitaji karavati, mvua ikinyesha wananchi,wanafunzi, wanavuka barabara kwa shida kwasababu maji yanajaa na kusababisha wakati mwingine wanafunzi kushindwa kupita kwenda shuleni wanakaa utoro au wanasubiri kwa saa kadhaa maji yapungue ndio wavuke kwenda shuleni’’ anasema Shija.

Shabani Nkungu ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM ) Tawi la Bujingwa anaipongeza Serikali kupitia TARURA kukarabati barabara na kusema kuwa ubovu wa barabara uliwatesa kisiasa na kuipa hofu CCM.

    Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM ) Tawi la Bujingwa, Shaban Nkungu akionesha ubovu wa barabara wakati haijakarabatiwa

'' Naishukuru Serikali inayoongzwa na CCM kwa usikivu tulilalamika na imesikiliza kilio chetu na kukarabati barabara ambayo ilitutesa kisiasa, tulipigwa madongo na wananchi wakiwemo wapinzani wakisema kuwa CCM imeshindwa kusimamia serikali ikarabati barabara.

'' Sasa tunachoomba TARURA ikamilishe zile kasoro zilizosalia iweke mitaro na karavati kwenye maeneo korofi ya barabara hiyo ili barabara iendelee kuwa imara. Inaleta faraja pale wananchi wakitoa kero zao na Serikali ikawajibika na kuzitatua''anasema.

Neema Joseph anasema kukarabatiwa kwa barabara kumerahisisha usafiri ''Baada ya barabara kukarabatiwa sasa hivi tunatumia nauli Tsh. 1000 kutoka Igombe senta hadi Bujingwa.

'' Wakati barabara haijatengenezwa ili ufike Bunjingwa ulilazimika kulipa Tsh. 3,000 na ukiwa na mgonjwa nyakati za usiku nauli ni zaidi ya Tsh.10,000 kwenda kituo cha afya Karume'' anasema Neema.

Mkazi wa mtaa wa Kilabela Kata ya Bugogwa, Lucy Samsoni anaipongeza TARURA kwa kukarabati barabara na kusema kuwa imewapunguzia mwendo na gharama kuzunguka sabasaba wanapokwenda wilayani.

         Muonekano wa barabara ya Igombe -Kahama mtaa wa Bujingwa kabla ya kukarabatiwa

''Baada ya barabara kukarabatiwa hatusumbuki tena kuzunguka sabasaba kwenda wilayani, tunapita hii hii barabara ya Igombe- Kahama muda mfupi umeshafika wilayani  kwa usafiri wa pikipi au bajaji kwa ghama ndogo ya Tsh. 1000 hadi 2000.

'' Wakati barabara haijakarabatiwa wakazi wa kata ya Bugogwa ili uende wilayani ulilazimika kupanda gari nauli Tsh. 1000 ushukie sabasaba ulipe tena nauli gari za kwenda Busweru wilayani Tsh. 600 jumla kwenda na kurudi ni Tsh. 3200, unatumia muda mwingi kwenda wilayani '' anasema Lucy Samson.

David Shija Mwendesha pikipiki anasema baada ya barabara kukarabatiwa imewapunguzia kero wanaposafirisha abiria kwani walipofika maeneo korofi abiria alilazimika kushuka kutembea kwa miguu hadi watakapofika eneo lisilo korofi.

        Muonekano wa barabara insyopita jirani na Nyumba ya Mwenyekiti wa CCM Tawi la Bujingwa kabla ya kukarabatiwa.

'' Kwakweli naishukuru Serikali kwa kukarabati barabara imetusaidia sana maana tulikuwa tukifika kwenye makorongo inabidi abiria ashuke atembee kwa miguu hadi sehemu ambayo barabara ina unafuu ndiyo apande tuendelee na safari.

''Kitendo hicho kiliwakera sana abiria maana katumia nauli yake alafu unamshusha atembee kwa miguu kisa tu ubovu wa barabara. Hali hiyo ilisababisha madereva wa pikipiki au bajaji kupandisha nauli kwa bei atakayojisikia’’ anasema David.

Mwendesha pikipiki huyo anasema kuwa bado kuna changamoto ya ukosefu wa karavati na mitaro na kwamba fedha zilizotengwa na TARURA kukarabati,kujenga mitaro na karavati ni ndogo kutokana na hali ya ubovu wa barabara hiyo hasa msimu wa mvua barabara uharibika sana na kuwa kero.

        Muonekano wa barabara ya Igombe -Kahama kabla haijakarabatiwa

'' TARURA ituwekee mitaro hii inasaidia mvua ikinyesha maji hayapiti juu ya barabara na haiharibiki mapema. Waweke na karavati maaana mvua ikinyesha nyingi maji yanajaa barabara inafunikwa na maji tunashindwa kusafirisha abiria pamoja na mizigo’’ anasema David.

Anaongeza kusema '' Nilisoma habari ya ubovu wa barabara ya Igombe- Kahama kwenye chombo hiki cha habari cha DIMA Online, Meneja TARURA anasema kuwa wametenga fedha Tsh. Milioni 25 kukarabati barabara, kuweka, karavati tano na mitaro mita 300 barabara  yenye urefu wa km 9.2.

‘’Mimi si mtaalamu wa mambo ya barabara lakini kwa kuona kwangu na mtumiaji wa barabara hii kwa miaka mingi hicho kiasi ni kidogo sana kufanya mambo yote hayo. Kiasi hicho naona ni cha ukarabati wa barabara tu.

'' Hakitoshi kuweka mitaro na karavati ndio maana unaona hiii barabara imekarabatiwa haijawekwa mitaro na karavati. Ni vema Serikali iongeze fedha ili ifanye kazi kwa uhakika barabara iwe imara’’ anasema David.

Barabara ijengwe kwa kiwango cha Lami

Mwenyekiti wa CCM Tawi la Bugogwa Shabani Nkugu anasema ili kuepusha gharama za mara kwa mara za ukarabati wa barabara ya Igombe – Kahama kuna haja ya Serikali kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami kwakuwa ni barabara muhimu inayokwenda hadi wilayani na Halmashauri.

Anasema kuwa barabara hiyo ikijengwa kwa kiwango cha lami itakuza uchumi wa mwananchi na serikali na itawaepushia gharama na muda wananchi wanaolazimika kupita barabara ya Igombe- mjini inayopita sabasaba wanapokwenda wilaya ya IIlemela na Halmashauri.

'' Hii barabara ikijengwa kwa kiwango cha lami itaharakisha maendeleo watu watajenga, magari mengi yatapita mazao yatasafirishwa bila shida, wavuvi wataneemeka maana wanapata shida kusafirisha samaki pindi barabara inapokuwa mbovu '' anasema Mwenyekiti CCM.

Kauli ya Meneja TARURA

Awali akizungumza na Mwandishi wa Habri wa DIMA Online ofisi ya TARURA, Meneja Wakala wa Barabara za Vijijini na Mjini (TARURA) wilaya ya Ilemela Mhandisi Sobe Makonyo kama ilivyoripotiwa katika chombo hiki cha habari Agosti, 26,2024 alisema kuwa barabara hiyo itakarabatiwa kwa kiwango cha changarawe, kujenga mitaro na karavati.  

        Meneja TARURA wilaya ya Ilemela Mhandisi Sobe Makonyo

Akaongeza kusema kuwa, Kazi kubwa zitakazofanyika ni kuikarabati ,kuweka karavati tano, mitaro mita 300 hasa sehemu korofi ili ziendelee kupitika ‘’ anasema Sobe.

Kuhusu ombi la wananchi la barabara kujengwa kwa kiwango cha lami, Sobe akasema kuwa ujenzi wa barabara hiyo utagharimu zaidi ya Bilioni 5, hivyo pesa zikipatikana itajengwa kwa kiwango cha lami.

Meneja TARURA akaeleza manufaa ya barabara hiyo kwamba ikifanyiwa matengenezo itarahisisha wanafunzi kwenda shuleni bila kupata adha , itavutia watu kuwekeza kandokando ya Kahama na Igombe na itachochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

'' Kazi ipo katika hatua ya manunuzi itakapokamilika kazi ya matengenezo itaanza mara moja . Barabara hiyo ni muhimu itawarahisishia wavuvi wa Igombe kufikisha mazao yao sokoni maana makao makuu ya wilaya yapo Busweru hivyo itasaidia kupunguza gharama na muda kuzunguka Sabasaba.

Kata ya Bugogwa ni miongoni mwa kata 19 ndani ya halamshauri ya Manispaa ya Ilemela, mkoa wa Mwanza. Ina jumla ya mitaa 19, kwa mujibu wa sensa ya  mwaka 2022, kata hiyo ina jumla ya kaya 7,108 zenye jumla ya wakazi 38,698 kati yao wanawake ni 22,666 na wanaume ni 16,032.

Mwezi Agosti, 26, 2024 DIMA Online iliripoti Makala iliyokuwa ikielezea namna barabara ya Igombe – Kahama inavyowapa mateso wananchi kutokana na ubovu wa barabara. Kwa undani wa Makala hiyo tembelea chombo hiki cha habari kupata undani wa Makala hiyo.

DIRA WIZARA YA UJENZI : Kuwa na miundombinu bora na endelevu itakayochochea maendeleo ya kiuchumi na kijamii nchini.





No comments