HEADER AD

HEADER AD

WAZIRI MKUU WETU, HONGERA ZIFIKE KWAKO

 


WAZIRI mkuu wetu, hongera zifike kwako,

Mekuwa kinara kwetu, ukifanya kazi zako,

Sasa kwenye Bunge letu, wamaliza muda wako,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Alishasema zamani, hata kumbukumbu ziko,

Ukiwa madarakani, unafanya ya mashiko,

Iingie akilini, kutambua muda wako,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Miaka kumi na tano, mbunge Ruangwa huko,

Na tano ongeza tano, kwa nafasi uliyoko,

Muda unatosha mno, hayo maamuzi yako,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Umefanya kazi zako, kwa huo uwezo wako,

Kwa zote nafasi zako, ulifanya ya mashiko,

Kweli kumbukumbu zako, zitazidia kuweko,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Kama Waziri Mkuu, takumbuka mambo yako,

Jinsi umekuwa juu, kwa usimamizi wako,

Wazembe wakuukuu, walionja joto lako,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Ruangwa hawajachoka, ungelitaka kuweko,

Lakini unaondoka, na watu machozi yako,

Ni jema limetendeka, huo uamuzi wako,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Msimamizi mahiri, ni moja ya sifa zako,

Kila jambo wahariri, ushahidi ukiweko,

Mefanya mengi mazuri, kapate mapumziko,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Nani asiyekumbuka, ufwatiliaji wako,

Jinsi walivyoumbuka, walioleta vituko,

Kula pesa kutibuka, sheria kuwa kiboko,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Sana tutakukumbuka, huo uongozi wako,

Na kila ukisikika, hayo matamko yako,

Vema umewajibika, acha pensheni iweko,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Ni mwanamichezo nguli, hiyo pia sifa yako,

Na tena kocha kamili, soka ni mapenzi yako,

Ona uwanja kamili, Ruangwa chagizo yako,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Darasa unalitoa, wanasiasa wenzako,

Muda  wanaoutoa, wakitumikia huko,

Ya kwamba kujiondoa, ndio ukomavu wako,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Ruangwa ajaye Bunge, mwanzo mwema takuwako,

Kwa Majaliwa atinge, na ushauri uweko,

Akienda akalonge, mazuri yenye mashiko,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Heri tunakutakia, kwenye ustaafu wako,

Uzidi kufurahia, pamoja na nyumba yako,

Huku ukitupatia, hiyo hekima ya kwako,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Nawe ni historia, ukuu miaka yako,

Wawili mmetimia, na Sumaye kaka yako,

Kumi kututumikia, hongera kwake na kwako,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Mungu alokuwezesha, kufanya mamuzi yako,

Azidi kupa maisha, furahia jasho lako,

Afya kikuneemesha, kwa miaka mingi yako,

Kung’atuka unapendwa, hilo jambo la maana.


Na Lwaga Mwambande (KiMPAB)

lwagha@gmail.com 0767223602

No comments