HEADER AD

HEADER AD

MAKAMU WA RAIS KUKABIDHI WAKIMBIZA MWENGE 2025

Na Gustaphu Haule , Pwani 

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Philip Mpango anatarajia kuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa ambapo pia atakabidhi vijana sita watakaokimbiza mwenge nchini.

Uzinduzi huo utafanyika katika viwanja vya Shirika la Elimu Tumbi Kibaha mkoani Pwani April 2,2025 ambapo vijana sita wanatoka Tanzania Bara na Tanzania visiwani.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu,Kazi ,Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu  Ridhiwani Kikwete ambaye pia ni mbunge wa Jimbo la Chalinze ,ametoa taarifa hiyo  Machi 26,2025 wakati akizungumza na Waandishi wa habari mjini Kibaha.

      Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu,Kazi,Vijana ,Ajira na Wenye Ulemavu Ridhiwani Kikwete (MB) akitoa taarifa ya maandalizi ya uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa kwa Waandishi wa habari leo Machi 26,2025 Mjini Kibaha.

"Ninayofuraha kuwajulisha wananchi kuwa Makamu wa Rais Dkt.Philip Mpango atakuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa utakaofanyika April 2,2025 katika viwanja vya Shirika la Elimu Tumbi Kibaha Mkoani Pwani,"amesema Ridhiwani. 

Amesema jukumu la kuukimbiza Mwenge wa uhuru utapita katika mikoa 31 yenye jumla ya Halmashauri 195 za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa siku 195.

Ameongeza kuwa katika kipindi chote Mwenge wa Uhuru utafanya kazi ya kuhamasisha amani,umoja, upendo na mshikamano wa Kitaifa na pia utawahimiza wananchi kushiriki shughuli za maendeleo ya kijamii na kiuchumi katika maeneo yao ya Halmashauri.

     Kikao cha Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Ridhiwani Kikwete kuhusu taarifa ya maandalizi ya uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru utakaofanyika April 2,2025 katika viwanja vya Shirika la Elimu Tumbi Kibaha Mkoani,kikao hicho kilifanyika Machi 26 Mjini Kibaha.

Amesema kuwa Mwenge wa Uhuru mwaka huu umebeba kauli mbiu ambayo ni Jitokeze kushiriki Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2025 kwa amani na Utulivu ujumbe ambao unalenga kuwaelimisha na kuwakumbusha Wananchi wote wa Tanzania kushiriki kikamilifu katika uchaguzi Mkuu wa amani na Utulivu.

Ameongeza kuwa sambamba na ujumbe mkuu wa mbio za Mwenge wa Uhuru pia Mwenge wa Uhuru utatumika kuelimisha Wananchi juu ya masuala ya kisekta na kisera katika muktadha wa Kitaifa na kimataifa ikiwa pamoja na kuendeleza juhudi za Kupambana na maradhi yanayotishia ustawi wa watu ikiwemo Ukimwi 

Mbali na ukimwi lakini pia juu ya masuala ya Kupambana na matumizi ya dawa za kulevya na vitendo vya rushwa  na katika Halmashauri zote utakapokuwa Mwenge wa Uhuru utaendelea kuwaelimisha Wananchi juu ya umuhimu wa Lishe Bora kwa afya njema.
    Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu Ridhiwani Kikwete ( katikati) akitembelea viwanja vya Shirika la Elimu Tumbi Kibaha.

Ridhiwani ametoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Pwani na mikoa jirani na watanzania kwa ujumla kujitokeza kwa wingi katika uwanja wa Shirika la Elimu Tumbi Kibaha mkoani Pwani ili April 2,2025  waweze kuungana na Dkt.Mpango katika uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru.

Ameipongeza kamati ya maandalizi ya uzinduzi wa mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa iliyochini ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani kwa kazi nzuri iliyofanyika na kuitaka kamati hiyo kumalizia sehemu iliyobaki.

Mkuu wa mkoa wa Pwani amemshukuru Waziri Kikwete kwa kutembelea katika uwanja huo na kwamba ameahidi katika siku zilizobaki kila kitu kitakuwa sawa.

     Mkuu wa Mkoa wa Pwani Abubakar Kunenge (kushoto)akimueleza jambo  Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu ,(MB) Ridhiwani Kikwete aliyetembelea viwanja vya Shirika la Elimu Tumbi wilaya ya Kibaha 


No comments