HEADER AD

HEADER AD

DORKASI NYAMONGO SDA, NYANGOTO SDA, FAMILIA YA MCHUNGAJI EAGT WATOA MSAADA KWA WASIOONA TARIME



>> Nguo, sabuni, fedha zatolewa

>> Afisa Maendeleo Kata ya Matongo, Kemambo nao waguswa

>> TLB Tarime wawashukuru wadau

Na Mwandishi Wetu ,Tarime

MAANDIKO Matakatifu katika Biblia, kitabu cha Luka 3 fungu la 11 kinasema “ Akawajibu akiwaambia ,Mwenye kanzu mbili na ampe asiye ma kanzu; naye aliye na vyakula na afanye vivyo hivyo”.

Kitabu hicho cha Luka 14 :13-14 kinasema “ Bali ufanyapo karamu waite maskini,vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri ,kwakuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufo wa wenye haki “.

Pia kitabu cha Matendo 9 : 36 kinasema “Na mwanafunzi mmoja alikuwako Yafa, jina lake Tabitha , tafsiri yake ni Dorkasi (yaani paa); mwanamke huyu alikuwa amejaa matendo mema na sadaka alizozitoa”.

Katika kutekeleza maandiko matakatifu ya Biblia , kikundi cha huduma ya wanawake (Dorkasi) katika kanisa la Waadventista Wasabato , Nyamongo Kati na Dorkasi katika kanisa la Nyangoto SDA wilayani Tarime ,mkoa wa Mara wametoa msaada wa fedha ,sabuni na nguo kwa wanachama wa chama cha wasioona (TLB) wilaya ya Tarime.

Kikundi cha Dorkasi Mei, 30, 2025 walifika katika ukumbi wa Ingwe sekondari -Nyamongo wakati wa mkutano wa wanachama wasioona waliokutana kwa ajili ya kujadili mambo ya chama kwa kipindi cha mwaka mzima.

       Wasioona wakiwa kwenye mkutano

Katika mkutano huo walihudhulia pia wadau mbalimbali akiwemo afisa maendeleo ya jamii kata ya Matongo Neema Abel , afisa maendeleo ya jamii kata ya Kemambo Mary Kitesho Laizer, afisa ustawii wa jamii kata ya Matongo, Elias Masangora , Frola  Eliud ambaye ni mke wa mchungaji  Eliud Wilson wa kanisa la EAGT Nyamongo ,na kutoa msaada.

Mwenyekiti wa Dorkasi Nyamongo Kati SDA , Sara Jonathani amesema Dorkasi ni kikundi kilichopo ndani ya kanisa kinachosaidia watu wenye uhitaji na kinasaidia hata walio nje ya kanisa la Waadventista Wasabato.

        Kikundi Cha Dorkasi kanisa la Waadventista Wasabato Nyamongo Kati wakiimba.

“Abia Orindo alitupatia mwaliko tukaona tuje tujumuike pamoja ,tumekuja na nguo, sabuni za unga zenye thamani ya Tsh. 60,000, pesa Tsh. 50,000 kwa ajili ya kutunisha mfuko wenu”amesema Sara.

“Kitabu cha Zaburi 34:18-19 kinasema Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo,na waliopondeka roho,na waliopondeka roho huwaokoa. Fungu la 19 linasema mateso ya mwenye haki ni mengi,lakini bwana humponya nayo yote”.

Kikundi hicho cha Dorkasi kikaimba wimbo wa kuwatia moyo wasioona wakisema kwamba, ni wajibu wa kila mtu kusaidia ,nyoosha mkono wako kwa wahitaji utabarikiwa na Mungu.

Wadau na Wanachama cha Wasioona wilayani Tarime wakiwa kwenye mkutano mkuu wa Chama hicho uliofanyika Nyamongo

Mwakilishi wa Dorkasi Nyangoto SDA , Ester Josephat Mwita, amewaomba wasioona kutokata tamaa kwani Mungu anawapenda jinsi walivyo huku akiwasisistiza kufanya kazi na kumwabudu Mungu na wakatoa Tsh. 50,000 kutunisha mfuko wa TLB na msaada wa nguo.

       Mwakilishi wa Dorkasi Nyangoto SDA , Ester Josephat Mwita akitoa msaada kwa Wasioona.

Flora Eliud mke wa mchungaji wa kaniasa la EAGT Nyamongo, Eliud Wilson amewatia moyo wasioona na kusema yupo pamoja nao huku yeye na familia yake wakichangia fedha na nguo  na kuahidi kuendelea kusaidiana na kikundi hicho.

Msaada huo wa wanawake ukamgusa afisa maendeleo ya jamii kata ya Matongo, Neema Abel na kutoa Tsh. 50,000 kwa ajili ya TLB huku afisa Maendeleo Kata ya Kemambo ,Mery Laizer akiwagusa kwa Tsh. 30,000 na kuahidi ushirikianao na chama hicho.

      Afisa maendeleo ya jamii kata ya Matongo, Neema Abel akitoa fedha kwa ajili ya kusaidia Chama cha Wasioona wilaya ya Tarime

Afisa Ustawi wa Jamii Kata ya Matongo, Elias Masangora,amesema afisa ustawi wa Jamii ni msimamizi mkuu kwa watu wenye ulemavu kwenye halmashauri na kwamba kata hiyo haikuwa na afisa ustawi wa jamii hivyo ameahidi kushirikiana na chama hicho.

     Afisa Ustawi wa Jamii Kata ya Matongo, Elias Masangora, akizungumza na wanachama wa chama cha Wasioona Tarime.

Mtunza hazina wa TLB Wilaya ya Tarime Bhoke Orindo amewashukuru Dorkasi Nyamongo , Dorkasi Nyangoto, familia ya mchungaji Eliud, mchungaji Alex Matiko, na wadau kutoka Nyamongo akiwemo Mkurugenzi kampuni ya WARACHA Daud Tindo ambaye ni mlezi wa kikundi hicho kwa kuwa bega kwa bega na kikundi hicho.

         Mweka Hazina Chama cha Wasioona wilaya ya Tarime, Bhoke Orindo akizungumza, kulia ni Flora Eliudi.

“Daud Tindo amekuwa akitusaidia sana kuhakikisha kikundi kinasonga mbele, Pia Mkurugenzi kampuni ya Rin, Isaack Range, KEMANYANKI, Gody Kubyo, John Jonathan, Maswa Sasi.

" Tunamshukuru Mama wawili , Werema Christopher aliyetuchangia Tsh. 800,000 na wengineo kufanikisha kikao hiki wamekuwa karibu na sisi kuhakikisha Chama kinasonga mbele .

"Tunamshukuru pia afisa maendeo ya jamii Kata ya Matongo, na wa kata ya Kemambo pamoja afisa ustawi wa jamii  kata ya Matongo tunapowaalika wanafika na kutupa ushirikiano.

Ameongeza kusema "Tunamshukuru  mkuu wa wilaya ya Tarime Gowele ambaye alikuwa ndio mkuu wa wilaya wa kwanza kufika kwenye kikao chetu cha wasioona na kuendesha harambee iliyofanikisha zaidi ya Tsh. Milioni 8 kuchangwa huku yeye akituchangia Tsh, Milioni moja, tunampenda sana tunomba siku nyingine atutembee , lakini pia uongozi wa shule ya Sekondari Ingwe ambao umekuwa ukitupatia ukumbi bure kufanya vikao vyetu “ amesema Bhoke.

Mwenyekiti wa Chama cha wasioona wilaya ya Tarime Museti Mwita , amewashukuru wadau wote ambao wamekuwa wakishirikiana na chama hicho ikiwemo kufanikisha vikao vya chama, ukiwemo uwezeshaji wa gharama za usafiri, chakula pindi wanachama wanapokutana kujadiliana masuala ya chama.

 

   Mwenyekiti wa Chama cha wasioona wilaya ya Tarime Museti Mwita akizungumza.

“Tunawashukuru wadau wote mnaotuunga mkono hakika tunapata faraja sana tunapoona mnatushika mkono. Tunamshukuru mwandishi wa Habari makini Dinna Maningo ambaye amekuwa mstari wa mbele kuripoti Habari za watu wasioona.

“Mungu akubariki sana kwa jitihada na akili zote unazotumia kwa ajili ya kuipaisha TLB,kupitia wewe TLB Tarime imeweza kufahamika. Bila nguvu za waandishi wa habaritusingefika hapa, maana wanaturusha na kazi zetu zinaonekana bila waandishi wa Habari watu wasingejua yanayofanywa na TLB” amesema Mwenyekiti.

Chama cha TLB kikamtunuku cheti cha shukrani mwenyekiti wa chama hicho mkoa wa Mara , Nyamlanga Rwakatare kwa ushirikiano Madhubuti na TLB wilaya ya Tarime.

      Mwenyekiti wa Chama cha wasioona mkoa wa Mara , Nyamlanga Rwakatare akiwa ameinua juu cheti cha pongezi alichotunukiwa na Chama cha Wasioona wilaya ya Tarime, akiwa amekishikilia yeye na afisa maendeleo ya jamii kata ya Kemambo, Mary Laizer.

        Afisa maendeleo ya jamii kata ya Kemambo, Mary Laizer akizungumza.

          Afisa Maendeleo kata ya Matongo, Neema Abel akizungumza.












No comments