HEADER AD

HEADER AD

SHAIRI: MIMI NIKO NA MANESI - 2

MIMI niko na manesi, kwenye zetu taasisi,

Yangu chanya siyo hasi, si uzushi ni halisi,

Wanavyotutunza sisi, afya napokuwa hasi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.


Daktari na manesi, wote watufaa sisi,

Tunapopata mkosi, afya kuwa na nakisi,

Wanavyotuenzi sisi, mimi nao sina kesi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.


Kama afya ni sisisi, hao watu wako nasi,

Hao wanashinda nasi, kuziandama tetesi,

Lugha zetu ukakasi, wavumilivu manesi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.


Ni wauguzi manesi, ile maana halisi,

Wanachukua nafasi, kututia moyo sisi,

Hata mambo yawe hasi, wala hawana uasi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.


Ni wakati kati ya sisi, kwa kutunzwa na manesi,

Walitumia nafasi, kupata ndoa na nesi,

Yale kwenye taasisi, nyumbani yawe halisi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.


Wewe muuguzi nesi, unayo kubwa nafasi,

Kazi yako si ususi, kumpendezesha Cesi,

Watu afya ziko hasi, wakutegemea nesi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.


Uchangamfu manesi, kwetu wagonjwa juisi,

Tamu kuliko nanasi, hata mwingine msosi,

Ule wetu ukakasi, unatoweka manesi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.


Inapotokea kesi, kuwahitaji manesi,

Ladha nzuri yenu kasi, mkitujia manesi,

Faraja toka utosi, hadi unyayo manesi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.


Msituchoke manesi, kwa maneno yetu hasi,

Hata yakija matusi, hiyo shida yetu sisi,

Magonjwa kwetu mkosi, hutufanya tuwe fisi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.


Ila tukipona sisi, kuwakumbuka manesi,

Miongoni mwetu sisi, tunaondoka kwa kasi,

Hata tupate nafasi, hatuwaenzi manesi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.


Mtusamehe manesi, majina yenu manesi,

Hayo hatushiki sisi, huo ni wetu uasi,

Waganga siyo manesi, ndio twawajali sisi,

Hongera kwenu manesi, hiyo huduma halisi.

Na Lwaga Mwambande (KiMPAB)

lwagha@gmail.com 0767223602

No comments