HEADER AD

HEADER AD

DC KIBAHA : IDARA YA ARDHI MMEKABIDHIWA GARI LITUMIENI KUTATUA CHANGAMOTO ZA WANANCHI KWA WAKATI

Na Gustaphu Haule, Pwani

MKUU wa Wilaya ya Kibaha Nickson Saimon amekabidhi  gari jipya kwa kitengo cha ardhi cha Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha ikiwa ni kuongeza ufanisi wa kuwafikia wananchi kwa haraka zaidi katika utatuzi wa changamoto za ardhi.

Makabidhiano hayo yamefanyika Desemba 1, 2025 katika viwanja vya ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa ya Kibaha na kuhudhuriwa na viongozi pamoja na  watendaji mbalimbali wa Serikali.

Akizungumza wakati wa kukabidhi gari hilo Saimon amesema hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, ambaye ameweka kipaumbele katika utatuzi wa migogoro ya ardhi na upatikanaji wa maeneo ya viwanda na uwekezaji.

     Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Nickson Saimon (kushoto) akimkabidhi mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dkt.Rogers Shemwelekwa (Kulia)funguo ya gari mpya kwa ajili ya idara ya ardhi ya Manispaa hiyo , hafla hiyo imefanyika Disemba 1/2025 katika viwanja vya Manispaa hiyo.

“Hili gari limeletwa ili muweze kuwafikia wananchi kwa haraka na kuhakikisha changamoto za ardhi zinatatuliwa kwa wakati kwahiyo nawaomba mlitunze na mlitumie kwa kazi iliyokusudiwa,”amesema Saimon.

Aidha, mkuu huyo wa Wilaya amempongeza mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha  Dkt. Rogers Shemwelekwa kwa kutekeleza maagizo kwa ufanisi huku akimuomba aendelee kufanyakazi kwa ajili ya kuwasaidia Wananchi.

         Hili ni gari jipya la idara ya ardhi katika Manispaa ya Kibaha Mkoa wa Pwani.

Awali, akiwasilisha taarifa fupi kwa mkuu wa Wilaya mkurugenzi wa Manispaa hiyo Dkt. Shemwelekwa amebainisha kuwa gari hilo linathamani ya sh. milioni 170 na litakuwa nyenzo muhimu katika kuongeza kasi ya utoaji huduma bora hususan katika idara ya Ardhi.

Mkuu wa idara ya Ardhi ya Manispaa ya Kibaha Denis Kahumba amesema changamoto ya usafiri ambayo ilikua ikikwamisha utendaji kazi sasa imepatiwa ufumbuzi.

“Ahadi yangu ni kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi kwahiyo ninashukuru kwa kupata kitendea kazi na kuweka  mazingira mazuri ya kazi ambayo yameongeza morali kwa watumishi,wa idara ya Ardhi ,” amesema  Kahumba.

      Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Nickson Saimon wa kwanza kushoto akizungumza na wakuu wa idara wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha katika hafla fupi ya makabidhiano ya gari jipya la idara ya ardhi ya Manispaa hiyo .

Naye kamishna msaidizi wa ardhi wa  Mkoa wa Pwani Rugambwa Banyikila, ametoa pongezi kwa uongozi wa Manispaa ya Kibaha kwa kutatua changamoto zilizokuwa zikikabili ofisi ya ardhi na kuwataka watumishi kuongeza bidii na uwajibikaji

Hata hivyo,Banyikila amesema makabidhiano hayo yanatarajiwa kuongeza kasi ya usimamizi wa ardhi, kutatua migogoro, na kuimarisha huduma kwa wananchi wa Kibaha  yakiendana na dira ya Serikali ya kujenga mazingira bora ya uwekezaji na maendeleo.

         Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Nickson Saimon ( kushoto), Mkurugenzi wa Manispaa ya Kibaha Dkt.Rogers Shemwelekwa (katikati) pamoja na Mkuu wa idara ya ardhi ya Manispaa ya Kibaha Denis Kahumba( Kulia) wakiwa katika hafla ya makabidhiano ya gari mpya ya idara ya ardhi ya Manispaa hiyo.


No comments