SHAIRI : MBINGU
MBINGU kaisimamisha, bila nguzo kutumia,
Kazi yake inatosha, kwa hilo twajivunia,
Kwetu amesadikisha, ana uwezo Jalia,
Kwa Mola hakuna zito yote yanawezekana.
Mbingu haina viraka, wala haijapasuka,
Imeumbwa kwa miaka, yenyewe imejishika,
Ni uwezo wa Rabuka, imara aliiweka,
Kwa Mola hakuna zito yote yanawezekana.
Mvua inatupatia, mashambani twalimia,
Mazao twajipandia, ardhini yanakua,
Kaliweka jua pia, kukaushia mimea,
Kwa Mola hakuna zito yote yanawezekana.
Siku sita katumia, mbingu kuikamilisha,
Mbingu akaisifia, na kisha kudhihirisha,
Sifa akaipatia, kwa kazi kukamilisha,
Kwa Mola hakuna zito yote yanawezekana.
Namaliza kuandika tumuabudu Manani,
Mengi nimeyaandika, tujifunze kwa yakini,
Kituoni nimefika, Kudusi tumthamini,
Kwa Mola hakuna zito yote yanawezekana.
Mtunzi Sir Dody Dody
Mudio islamic seminary
Moshi, Kilimanjaro
0671159555

Post a Comment