POLISI KAGERA YAPIGA MARUFUKU DISCO TOTO

Na Alodia Dominick, Bukoba
JESHI la polisi mkoani Kagera limepiga marufuku disco la watoto wakati wa kusherekea sikukuu za Idi na Pasaka ili kuwaepusha na madhara ambayo yamekuwa yakijotokeza siku za nyuma pindi wanapokuwa kwenye kumbi za disco hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari, kamanda wa polisi mkoa wa Kagera Blasius Chatanda ofisini kwakwe amesema jeshi hilo mpaka sasa hawajapokea taarifa kutoka kwa mtu yoyote ya kuomba kibali ili kuendesha biashara hiyo ya disco toto hivyo, ni marufuku mtu yeyote kufanya hivyo.
Amesema malezi na ulinzi wa mtoto unaanzia nyumbani hivyo amewataka wazazi na walezi kutowaachia watoto kwenda matembezi peke yao siku hizo ili kuwaweka salama muda wote.
Kamanda Chatanda amesema wazazi kuachia watoto bila uangalizi siku za sikukuu inaweza kuhatarisha usalama wao ikiwemo kugongwa barabarani na watumiaji wa barabara wasiozingatia sheria za usalama barabarani au hata kuzama kwenye maji ikiwa watajaribu kuogelea katika fukwe za ziwa.
Vilevile kamanda Chatanda ametoa onyo kwa waendesha vyombo vya moto kuepuka kuendesha nyakati za sikukuu wakiwa wametumia voleo kwani kufamya hivyo ni kukiuka sheria za usalama barabarani.
"Nawashauri wote wenye vyombo vya moto ukienda mahala ukanywa ukalewa usiendeshe kama ni gari,tupigie sisi polisi tutakusaidia na ukikiuka hiyo na ukaendesha basi ni kwamba utakuwa umedhamiria kwa hiyo tutakukamata na tutakuchukulia hatua kali za kisheria" amesema Kamanda Chatanda.

Post a Comment